MTOTO AFUNGIWA KWENYE BANDA LA MBUZI KWA MIAKA 10
Mwenyekiti
 wa Umoja wa Watu wenye Ulemavu Kenya, David Sankok akionyesha hali 
halisi ya maisha ya mtoto huyo kabla ya kuokolewa. Picha na Ndaya Mgoyo 
Juni 21 ilikuwa ni siku ya kawaida kwa Mama Nancy mkazi wa Narok nchini Kenya, lakini ilifichua siri nzito ya mtoto aliyefichwa kwa miaka kumi katika banda la mbuzi.
Akiwa katika shughuli zake za nyumbani, mara akatokea mtoto mdogo wa jirani yake aitwaye Jane.       
Binti huyo akaanza kucheza na wenzake kwa dakika kadhaa na mara akaacha michezo na kuanza kukimbia kuelekea nyumbani kwao.
Wenzake
 wakamuuliza “mbona unakimbia wakati bado tunacheza”. Akajibu, “nakwenda
 kwenye banda la mifugo kumpa chakula Ben. Muda umekimbia na hakuna mtu 
nyumbani”.
Kwa
 kauli hiyo, mwanamke huyo alitaka kujua iwapo Ben anaishi kwenye nyumba
 ya jirani yake kwani ni miaka 10 imepita tangu amtie machoni.
“Ben
 yupo na anaishi kwenye banda la mifugo. Huwa anahudumiwa na mama, 
lakini kwa sasa mama hayupo na baba amekwenda kazini. Mimi nina jukumu 
la kumpa chakula,” alijibu Jane.
Mama
 huyo akapata shauku ya kumtembelea mtoto huyo kuona kinachoendelea kwa 
jirani zake, Lo! anachokiona haamini macho yake; Mtoto Ben amefungwa kwa
 kamba kwenye kigodoro chembamba akiwa hajiwezi kwa njaa.
Hivyo ndivyo alivyoibuliwa mtoto Ben baada ya kukaa katika banda la mbuzi kwa muda wa miaka 10 bila majirani kufahamu.
Ben,
 ambaye kwa sasa ana miaka   miaka 14 alizaliwa akiwa kiziwi, bubu   na 
ulemavu. Aibu ya kuzaa mtoto kama huyo ndiyo ilifanya wazazi wake 
wamfungie kwenye zizi la wanyama kwa muda wa miaka 10 na wakihakikisha  
hakuna jirani wala ndugu wa karibu anayefahamu juu ya tukio hilo.
Historia ya mtoto huyo
Kwa
 mujibu wa baba mlezi Mr Jeremiah Mbusia,  ambaye ni askari katika 
Wizara ya Mali Asili, Narok Kenya, mtoto  huyo siyo wake wa kuzaa bali 
alifika katika nyumba hiyo miaka 12 iliyopita akiwa na mama yake wakati 
huo mtoto huyo alikuwa na miaka minne.
Alilelewa
 katika nyumba hiyo kwa miaka miwili na ndipo wazazi wake, yaani baba 
yake wa kambo na mama yake mzazi wakaamua kumuweka katika kibanda kidogo
 nje ya nyumba yao  na hutumiwa kama zizi la mbuzi na kondoo.
Maisha ndani ya  zizi
Akiwa kwenye zizi mtoto huyo aliwekewa godoro ukutani na mkono wake mmoja ulifungwa kwa kamba ukutani.
Ilikuwa
 ni vigumu kuvumilia harufu kali kutoka katika zizi hilo kwani kulikuwa 
na mchanganyiko wa kinyesi na mikojo ya binadamu na wanyama.
Wadogo
 zake Ben walisema kuwa wazazi wao huwa wanamsafisha mtoto huyo wakati 
wowote wanaotaka na kuwa anaweza kushinda na kinyesi au kulala nacho.
“Ni
 mara chache kukuta akisafishwa   mara mbili kwa siku. Kwa kawaida 
husafishwa mara moja tu na wakati mwingine hasafishwi kabisa,” alisema 
mtoto huyo.
Kwa nini ilikuwa rahisi kujulikana?
Ugunduzi
 wa mtoto huyo ulitokana na ukweli kwamba mama yake aliamua kuondoka 
nyumbani na kuacha familia nzima kutokana na ugomvi na mume wake.
Mama
 huyo alikuwa akifanya siri ya kulinda mtoto huyo asijulikane hapo 
nyumbani na alipoondoka watoto wenzake ndiyo walikuwa na jukumu la 
kumlisha mwezao.
Kauli ya baba mlezi
Kwa kujibu wa baba wa kambo, mama wa mtoto huyo alikuwa hamtaki mwanaye kwani aliamini kwamba kuishi naye ni kuongeza mikosi.
Baada
 ya kuishi pamoja walijikuta wakiwa wamezaa watoto watatu na mama huyo 
aliona kuwa watoto hao ndio walikuwa muhimu katika maisha yake kuliko 
Ben, ambaye alimzaa na mwanaume mwingine kabla ya kuolewa katika ndoa 
rasmi.
“Mama
 yake alikuwa hampendi na hata wazo la kumweka katika banda lilitoka 
kwake. Aliamini kuwa kukaa naye ndani kama watoto wa kawaida ilikuwa ni 
usumbufu na akitoa visingizio kwamba akikaa ndani anaweza kuvunja vitu 
na kuwa anaweza kushika vitu vya hatari kama vile moto,” alijitetea baba
 mlezi wa Ben.
“Tulikosana
 na mama watoto kwa ugomvi wa kawaida tu katika familia, hiyo ilikuwa ni
 miezi minne iliyopita, ajabu ni kwamba amenikimbia na kuniachia familia
 akiwamo mtoto mlemavu.” “Nashindwa kumlea vizuri kwa kuwa natakiwa 
kwenda katika mihangaiko yangu ndiyo maana wadogo zake walikuwa 
wakimhudumia wakati sipo.”
Imefahamika
 kuwa mwanamke huyo amekimbilia kwao eneo la Rimuru, Kenya ambapo ni kwa
 wazazi wake na akiwaambia jamaa zake wa karibu kuwa hawezi kurudi 
katika nyumba ya mume wake kwani hawapatani.
Kauli za majirani
Majirani
 wanasema walikuwa wakifahamu kuwa nyumbani kwa jirani yao kuna mtoto 
mwenye ulemavu wa akili lakini hawakumwona kwa muda mrefu.
“Tulikuwa
 tukifahamu kwamba kuna mtoto mlemavu wa akili lakini katika kipindi cha
 miaka 10 iliyopita hatukumwona. Tulidhani  wamemhamishia sehemu 
nyingine. Ilikuwani vigumu kusikia sauti kwa kuwa mtoto mwenyewe ni bubu
 na kiziwi,” alisema jirani mmoja.
Kumuokoa Ben
Baada ya majirani kupata taarifa za kuwepo kwa mtoto huyo, walimuita mwandishi wa habari mmoja ili kushuhudia hali halisi.
Mwandishi
 huyo alitoa taarifa polisi na pia kwa Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la 
watu wenye ulemavu Kenya, Dk David Ole Sankok  na kwa pamoja walivamia 
katika nyumba hiyo iliyopo Fanaka Estate, Narok na kumwokoa mtoto huyo 
katika mateso. 
Baada
 ya kumtoa kwenye kibanda hicho waligundua kuwa hali ya mtoto huyo  
haikuwa nzuri kwani alikuwa amepooza upande mmoja wa kushoto kutokana na
 kulala kwa muda mrefu, viungo vyake vilikuwa vimejikunja kutokana na 
kukosa lishe kwa siku nyingi na nywele zake zilibadilika rangi kutokana 
na kutokaa kwenye mwanga wa jua kwa muda mrefu.
“Alikuwa
 akitoa harufu kali, ilikuwa ni vigumu hata kumsogelea, lakini kwa kuwa 
tulikuwa tumedhamiria kumwokoa ilibidi tufanye hivyo,” akasema Dk Ole 
Sankok. “Tulimkuta katika mateso makubwa sana, eneo alilokuwa amelala 
lilikuwa na kunguni, chawa na viroboto wengi,” anasema.
Anaongeza kuwa wadudu hao walipokuwa wakimsogelea kinywani alikuwa akiwatafuna na kuwameza kwani alikuwa na njaa muda wote.
“Nilipoona
 hali hiyo nilijaribu kuondoa viroboto waliokuwa karibu na mdomo wake, 
kwa kuwa alikuwa amewazoea sana na aliona ni kama kitoweo chake alitoa 
sauti ya ukali kuashiria kwamba nisiwatoe, nilipojaribu kuwatoa kwa 
nguvu alitaka kuniuma kwa meno,” alisema daktari huyo.
Wazazi
 wa kijana huyo walikuwa hawaaniki godoro nje kwani hawakua na jingine 
la kumtandikia pia walihofia majirani huenda wangehoji.
Huduma ya kwanza
Baada
 ya kugunduliwa, Ben alipelekwa katika Hospitali ya Mji wa Narok kwa 
ajili ya matibabu. Alipewa huduma za haraka ikiwa ni pamoja na huduma za
 kurudisha afya mwilini kwa vyakula vya protini na vitamini.
Vilevile
 alikuwa akianikwa juani mara kwa mara kwa lengo la kumrudishai 
vitamini. Kwa kuwa mgongo wa mtoto huyo ulianza kutoa vidonda alipewa 
matibabu ya vidonda.
 “Mtoto
 huyo alikuwa amepungua mwili kwa kiasi kikubwa  ilikuwa unaweza kumbeba
 kama mtoto mdogo. Hata   rangi yake ya ngozi ilibadilika,” alisema Dk 
Sankok, ambaye pia anaendesha kliniki binafsi katika mji wa Narok.
“Licha ya kuwa na umri wa miaka 14 alikuwa na kilo 15 pekee,” aliongeza.
 Sankok
 aliwahakikishia watu waliomzunguka mtoto huyo kwamba atamfikisha katika
 kituo cha kulelea watoto wenye ulemavu wa akili na viungo na atampa 
mazoezi ya kutosha kuhakikisha anarudi katika hali ya kawaida.
“Unajua
 kuna wazazi ambao wana kawaida ya kuwaficha watoto wao kwa sababu wana 
matatizo ya viungo ama   ya akili. Hilo siyo jambo zuri hata kidogo, 
watoto kama hao ni binadamu wa kawaida na wanatakiwa kulelewa kwa 
misingi yote ya kibinadamu,” anasema.
Anasema
 kama mzazi anaona hawezi kumhudumia mtoto kama huyo ni bora amfikishe 
katika vituo vya kulea watu wa aina hiyo kuliko kumficha ndani na kumpa 
mateso makubwa.
 
 
  
 
hadi wakenya..mamaaa
ReplyDelete